Tuesday, April 9, 2013

Mapenzi Ya Kweli.



Wanaume waamue kupenda na kukubali mitihani ya namna yoyote itakayowakuta wapenzi wao. Wafanye kama alivyoweza Sajuki pale mwenzi wake Wastara alipopata ajali, akakatika mguu. Inawezekana tu kama unakuwa na moyo wa kweli.
 Wanawake washike njia ya Wastara. Maradhi au matatizo ya aina yoyote watakayoyapata wapenzi wao, kwao iwe ni changamoto ya kulazimisha kuivuka. Kuna heshima na baraka nyingi katika kufanya kama alivyotenda Wastara kwa Sajuki.
 Vilevile, ieleweke kuwa kuna laana katika kumkimbia mwenzi wako pale anapopatwa na matatizo. Hayakuumbwa majanga bila ya kuwepo kwa binadamu. Unaweza kumkimbia mpenzi wako kisa kapata ajali na kutokwa meno, wiki inayofuata nawe yakafika, ukawa chongo.
 Mwenzi baadaye anaweka meno ya bandia, anaweza kusimama mbele za watu na kutabasamu, wewe inakuwa ngumu, kwani jicho ndiyo hilo limekwenda zake. Kila mtu akiutakasa moyo wake na akapenda kikwelikweli, mapenzi yatakuwa rahisi mno.
 Ni somo tu, watu wajionee maisha jinsi yalivyo. Wakati Wastara anamvumilia Sajuki pamoja na mitihani mikubwa waliyokuwa nayo, wapo wanawake wanaopata kila wanachohitaji, fedha zipo lakini wanasaliti ndoa zao mchana kweupe.
 Jiulize wewe ndugu yangu, ni heshima gani ambayo Wastara anapewa leo hii? Kama angemfanyia Sajuki kinyume chake, kwa hakika hivi sasa angekuwa anasemwa vibaya sana. Kinyume cha heshima ni dharau. Nawe unaweza kuamua leo kwamba uheshimiwe au udharauliwe.
 Mtu anaweza kudhani kwamba Wastara alimkuta Sajuki akiwa na maisha mazuri pamoja na umaarufu wake. La hasha! Walikutana wakiwa wadogo lakini wakaunganisha ndoto na matarajio ya kufanikiwa pamoja. Malengo yao yalikuwa ya dhati ndiyo maana mwisho wao ukawa huo.
 Waliposema “kifo kitutenganishe”, walimaanisha kweli. Mitihani haikuwatenganisha mpaka Sajuki akatangulia mbele ya haki, Wastara akamzika, na sasa anakaa eda. Hicho ni kipimo thabiti kuwa waliamua kupendana kiukweliukweli. Ingekuwa wanafanya utani, wangeachana siku nyingi zilizopita.
 Kuuguza ni mtihani mzito hasa pale inapotokea kwamba mgonjwa mwenyewe anakuwa ameugua kwa muda mrefu. Zipo changamoto ambazo hujitokeza ndani, hususan pale mgonjwa mwenyewe anapoathirika kisaikolojia.
 Wapo ambao waliwasusa wagonjwa wao kwa sababu ya kuchoka maneno. Unaweza kufanya kile ambacho unakiona wewe ni kizuri lakini mwenyewe akahisi unamnyanyapaa. Wastara na Sajuki walikuwa marafiki mpaka Mungu alipotekeleza wito wake kwamba kila nafsi itaonja mauti.
 Mshikamano ambao waliuonesha ni urithi mkubwa hata kwa mtoto wao ambaye Sajuki amemuacha akiwa mdogo sana. Akikua, atapata simulizi ya namna ambavyo wazazi wake walishikamana kwa upendo katika vipindi vyote vya matatizo mpaka kifo kilipowatenganisha.
 Atawaona wazazi wake ni mashujaa kweli. Ni ukweli kuwa kama Sajuki angemsaliti Wastara alipopata ajali na kukatika mguu, vilevile mtoto huyo asingezaliwa. Ina maana kwamba upendo na mshikamano wao, vilisababisha mtoto Fahreen akazaliwa.
 Tujifunze sasa, Mungu huwa haiachi mitihani ije tu, bali huwa na maana yake. Unatakiwa kushikamana na mwenzi wako kwa hali na mali. Zipo sababu ambazo zinaweza kuwafanya muachane lakini isiwe matatizo. Kumuona mwenzi wako hakufai kisa hana fedha ni ujinga sana.
 Wewe mwanaume, umeona jinsi Sajuki alivyopewa taji la heshima kwa namna alivyohusika kimapenzi kwa Wastara. Wewe mwanamke, umejionea uvumilivu wa Wastara wakati wa matatizo ya Sajuki, basi sasa, wao wawe ni mfano kwako, pale unapohitaji kuona picha ya maana halisi ya mapenzi

No comments:

Post a Comment