Wanaume waamue kupenda na
kukubali mitihani ya namna yoyote itakayowakuta wapenzi wao. Wafanye kama
alivyoweza Sajuki pale mwenzi wake Wastara alipopata ajali, akakatika mguu.
Inawezekana tu kama unakuwa na moyo wa kweli.
Wanawake washike njia
ya Wastara. Maradhi au matatizo ya aina yoyote watakayoyapata wapenzi wao, kwao
iwe ni changamoto ya kulazimisha kuivuka. Kuna heshima na baraka nyingi katika
kufanya kama alivyotenda Wastara kwa Sajuki.
Vilevile, ieleweke
kuwa kuna laana katika kumkimbia mwenzi wako pale anapopatwa na matatizo.
Hayakuumbwa majanga bila ya kuwepo kwa binadamu. Unaweza kumkimbia mpenzi wako kisa
kapata ajali na kutokwa meno, wiki inayofuata nawe yakafika, ukawa chongo.
Mwenzi baadaye
anaweka meno ya bandia, anaweza kusimama mbele za watu na kutabasamu, wewe
inakuwa ngumu, kwani jicho ndiyo hilo limekwenda zake. Kila mtu akiutakasa moyo
wake na akapenda kikwelikweli, mapenzi yatakuwa rahisi mno.
Ni somo tu, watu
wajionee maisha jinsi yalivyo. Wakati Wastara anamvumilia Sajuki pamoja na
mitihani mikubwa waliyokuwa nayo, wapo wanawake wanaopata kila wanachohitaji,
fedha zipo lakini wanasaliti ndoa zao mchana kweupe.
Jiulize wewe ndugu
yangu, ni heshima gani ambayo Wastara anapewa leo hii? Kama angemfanyia Sajuki
kinyume chake, kwa hakika hivi sasa angekuwa anasemwa vibaya sana. Kinyume cha
heshima ni dharau. Nawe unaweza kuamua leo kwamba uheshimiwe au udharauliwe.
Mtu anaweza kudhani
kwamba Wastara alimkuta Sajuki akiwa na maisha mazuri pamoja na umaarufu wake.
La hasha! Walikutana wakiwa wadogo lakini wakaunganisha ndoto na matarajio ya
kufanikiwa pamoja. Malengo yao yalikuwa ya dhati ndiyo maana mwisho wao ukawa
huo.
Waliposema “kifo
kitutenganishe”, walimaanisha kweli. Mitihani haikuwatenganisha mpaka Sajuki
akatangulia mbele ya haki, Wastara akamzika, na sasa anakaa eda. Hicho ni
kipimo thabiti kuwa waliamua kupendana kiukweliukweli. Ingekuwa wanafanya
utani, wangeachana siku nyingi zilizopita.
Kuuguza ni mtihani
mzito hasa pale inapotokea kwamba mgonjwa mwenyewe anakuwa ameugua kwa muda
mrefu. Zipo changamoto ambazo hujitokeza ndani, hususan pale mgonjwa mwenyewe
anapoathirika kisaikolojia.
Wapo ambao waliwasusa
wagonjwa wao kwa sababu ya kuchoka maneno. Unaweza kufanya kile ambacho
unakiona wewe ni kizuri lakini mwenyewe akahisi unamnyanyapaa. Wastara na
Sajuki walikuwa marafiki mpaka Mungu alipotekeleza wito wake kwamba kila nafsi
itaonja mauti.
Mshikamano ambao
waliuonesha ni urithi mkubwa hata kwa mtoto wao ambaye Sajuki amemuacha akiwa
mdogo sana. Akikua, atapata simulizi ya namna ambavyo wazazi wake walishikamana
kwa upendo katika vipindi vyote vya matatizo mpaka kifo kilipowatenganisha.
Atawaona wazazi wake
ni mashujaa kweli. Ni ukweli kuwa kama Sajuki angemsaliti Wastara alipopata
ajali na kukatika mguu, vilevile mtoto huyo asingezaliwa. Ina maana kwamba
upendo na mshikamano wao, vilisababisha mtoto Fahreen akazaliwa.
Tujifunze sasa, Mungu
huwa haiachi mitihani ije tu, bali huwa na maana yake. Unatakiwa kushikamana na
mwenzi wako kwa hali na mali. Zipo sababu ambazo zinaweza kuwafanya muachane
lakini isiwe matatizo. Kumuona mwenzi wako hakufai kisa hana fedha ni ujinga
sana.
Wewe
mwanaume, umeona jinsi Sajuki alivyopewa taji la heshima kwa namna alivyohusika
kimapenzi kwa Wastara. Wewe mwanamke, umejionea uvumilivu wa Wastara wakati wa
matatizo ya Sajuki, basi sasa, wao wawe ni mfano kwako, pale unapohitaji kuona
picha ya maana halisi ya mapenzi